Korea Kaskazini yamzuia Ban kuitembelea nchi hiyo
Viongozi wa Korea Kaskazini wamefuta kibali walichokuwa wametoa kwa
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki moon, kutembelea eneo moja la
viwanda nchini humo.Akizungumza mapema leo mjini Seoul, Korea Kusini, Katibu Mkuu wa UN amesema wamepokea taarifa kutoka Pyongyang kwamba hawana idhini tena ya kutembelea eneo la viwandani la Kaesong lakini hawakupewa sababu za kufutwa kibali walichokuwa wamepewa.
Mwanadiplomasia huyo wa Umoja wa Mataifa amesema hatua hiyo ya Korea Kaskazini inasikitisha na kuvunja moyo. Kama angeingia Korea Kaskazini, Ban angekuwa Katibu Mkuu wa 3 wa UN kuizuru nchi hiyo.
Katibu Mkuu wa mwisho wa UN kuitembelea Pyongyang mwaka 1993 alikuwa Boutros Boutros-Ghali. Korea Kaskazini inatuhumiwa na jamii ya kimataifa kuwa na rekodi mbaya zaidi ya ukiukaji wa haki za binadamu duniani.
Viongozi wa nchi hiyo wanasema Marekani ndiyo inayoendesha propaganda na kupotosha ukweli wa mambo kuhusu hali ya haki za binadamu nchini humo.
Post A Comment
Hakuna maoni :