
Mjumbe wa Umoja wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo
amesisitiza kuwa, Nelson Mandela ameufanya ulimwengu kuwa eneo bora la
kuishi. Akizungumza jana Jumamosi kwa mnasaba wa Siku ya Kimataifa ya
Nelson Mandela Rais wa zamani wa Afrika Kusini, Martin Kobler amesema
kuwa Mandela ameifanya dunia kuwa mahala bora pa kuishi, na kwamba
Mandela anaendelea kuwa shakhsia wa kuigwa na watu wote. Mjumbe wa Umoja
wa Mataifa katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ameongeza kuwa:
Kutatuliwa mizozo na mivutano, kuuunga mkono haki za binadamu, kupambana
na ubaguzi wa rangi na kijinsia na kuanzisha umoja wa kitaifa, yote
hayo yanawezekana iwapo misingi ya Mandela itafuatwa. Nelson Mandela
Rais wa zamani wa Afrika Kusini alizaliwa tarehe 18 Julai mwaka 1918 na
aliaga dunia tareheh 5 Disemba mwaka juzi. Baraza Kuu la Umoja wa
Mataifa limetangaza tarehe 18 mwezi Julai kila mwaka kuwa ni Siku ya
Kimataifa ya Nelson Mandela kutokana na kujitolea kwake katika kueneza
utamaduni wa amani duniani kote. Mzee Nelson Mandela alifungwa jela
miaka mingi na utawala wa Wazungu wa Apartheid kutokana na kupigania
haki za raia weusi wa Afrika Kusini.
(chanzo tehran radio udhaa ya kiswahili)
Post A Comment
Hakuna maoni :