technology

“Jeshi la Sudan Kusini limefanya jinai kubwa”

“Jeshi la Sudan Kusini limefanya jinai kubwa”Waangalizi wa haki za binaadamu nchini Sudan Kusini wamelikosoa vikali jeshi la Sudan Kusini kwa kutenda jinai dhidi ya binaadamu nchini humo. Taarifa iliyotolewa leo la mashirika ya kutetea haki za binaadamu nchini humo yamelaani vitendo vya ukatili wa kupindukia dhidi ya raia wasio na hatia na yameitaka serikali ya Juba kuchunguza jinai hizo haraka iwezekanavyo. Mashirika hayo yamesema askari wa Sudan Kusini wamekuwa wakiwalenga na kuwakanyaga kwa vifaru raia wanaokimbia machafuko. Ripoti hiyo imeongeza kuwa, mashambulizi hayo ya kikatili yangali yanaendelea, suala ambalo linatia wasiwasi mkubwa.
Takwimu za Umoja wa Mataifa zinaonesha kuwa zaidi ya watu milioni mbili na laki mbili, raia wa Sudan Kusini wamelazimika kuyakimbia makazi yao ambapo laki sita kati yao wamekimbilia katika nchi jirani za Ethiopia, Kenya na Uganda. Ripoti hiyo ya Umoja wa Mataifa imeongeza kuwa, karibu asilimia 70 ya jamii ya watu milioni 12 wa Sudan wanakabiliwa na matatizo ya usalama wa chakula.
Sudan Kusini ilitumbukia katika machafuko tangu mwezi Disemba mwaka 2013 baada ya Rais Salva Kiir wa nchi hiyo kumtuhumu makamu wake wa zamani kwa kupanga njama ya kutaka kumpindua, machafuko ambayo yamepelekea maelfu ya watu kuuawa.

(chanzo tehran radio idhaa ya iswahil)
Post A Comment
  • Blogger Comment using Blogger
  • Facebook Comment using Facebook
  • Disqus Comment using Disqus

Hakuna maoni :