technology

Rwanda: Nchi za Magharibi zinatetea watenda jinai

Serikali ya Rwanda imekosoa vikali hatua ya kukamatwa mkuu wa shirika la ujasusi la nchi hiyo huko Uingereza kufuatia ombi la Uhispania na kusema nchi za Magharibi zimeshawishiwa na wale waliotekeleza mauaji ya kimbari nchini humo mwaka 1994.
Karenzi Karake, Mkuu wa Idara ya Usalama wa Taifa ya Rwanda alitiwa mbaroni Jumamosi iliyopita katika uwanja wa ndege wa Heathrow jijini London. Karenzi Karake mwenye umri wa miaka 54 alifikishwa katika mahakama ya Westminster baada ya kukamatwa kufuatia waranti uliotolewa na mahakama ya Uhispania, ambako anatafutwa kwa madai ya kuhusika katika jinai za kivita dhidi ya raia. Atarejeshwa tena mahakamani siku ya Alkhamisi.
Kufuatia tukio hilo Waziri wa Mambo ya Nje wa Rwanda Louise Mushikiwabo amesema ni jambo lisilokubalika kwa nchi za Magharibi kushirikiana katika kuwadhalilisha Waafrika. Katika taarifa aliyoiandika katika akaunti yake ya kijamii wa Twitter, Mushikiwabo amesema: 'Ni fedheha kumtia mbaroni afisa wa Rwanda kwa msingi wa uwendawazimu wa wanaounga mkono mauaji ya kimbari.' Kesi hiyo huwenda ikazorotesha zaidi uhusiano wa Rwanda na Uingereza baada ya wakuu wa Kigali kupiga marufuku nchini humo Idhaa ya Kinyarwanda ya BBC mwaka jana baada ya shirika hilo la utangazaji la serikali ya Uingereza kutilia shaka kauli rasmi kuhusu mauaji ya kimbari yaliyofanyika Rwanda mwaka 1994.
Post A Comment
  • Blogger Comment using Blogger
  • Facebook Comment using Facebook
  • Disqus Comment using Disqus

Hakuna maoni :